Washauriwa kuanzisha bustani za wanyama

Wafanyabiashara wakubwa nchini washauriwa kuchangamkia fursa ya kibiashara ya kuanzisha bustani za wanyama (Zoo).

Serikali imetoa wito kwa wafanyabiashara wakubwa nchini kuchangamkia fursa ya kuanzisha bustani za wanyama kwa lengo la kuwasogezea utalii wageni kutoka nje pamoja na kuiwezesha serikali kuongeza mapato katika sekta ya utalii.

Hayo yamesemwa na Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyapori (TAWA), Kanda ya Kaskazini, Peter Manyenga, alipokuwa akizindua bustani hiyo ya kisasa Kanda ya Kaskazini na kusema kuwa kufanya hivyo, kutaunga mkono jitihada za serikali kuhamasisha watalii kuja nchini.

Amesema TAWA iko kuhakikisha inaongeza mazao mapya hapa nchini, hususani zao la bustani ya wanyama kama hiyo ya Serval iliyopo, Wilaya ya Siha Mkoani Kilimanjaro, kwani biashara hiyo ni ngeni nchini tofauti na nchi jirani.

Amesema ni vyema wafanyabiashara na wadau wa utalii kuchangamkia fursa hiyo, ili serikali iweze kuongeza mapato zaidi.

Ameeleza kuwa bustani ya wanyama ya Serval ni kisasa, yenye wataalamu wa afya wenye kuzingatia kanuni, sheria na miongozo ya kutunza wanyama.

Meneja wa bustani ya wanyama ya Serval, Fahad Nassoro Hamudu, amesema uanzishwaji wa bustani hiyo ni kuitangaza Tanzania katika nchi za Kiarabu juu ya zao jipya la utalii hapa.

Amesema bustani hiyo ni tofauti na nyingine, kwani wanyama wote waliopo ni rafiki na binadamu na wanalishwa vyakula na kunyweshwa maji na binadamu

Likes:
0 0
Views:
1416
Article Categories:
UncategorizedWildlife