Kuhusu Kiboko

Kiboko ni miongoni mwa jamii ya wanyama ambao wanaishi muda mrefu sana kwenye maji ukilinganisha na mamalia wengine wote.

Anapenda kukaa kwenye maji kwasababu ngozi yake haina vinyweleo kabisa hivyo kushindwa kuhimili mionzi ya jua kwa hiyo maji humsaidia kupooza joto la mwili.

Kiboko hutoa maji maji yenye rangi nyekundu na watu huchanganya na kusema ni damu lakini si damu bali ni maji maji maalumu ambayo huyatoa ili kuulainisha mwili kutokana na athari zitokanazo na mionzi ya jua.

Kiboko ni mnyama msafi ambaye hawezi kujisaidia kwenye maji lakini pia hapendi kuguswa kwenye makalio yake hivyo huepuka samaki na wadudu wengine kumgusa wakati wa kujisaidia.

Macho na matundu ya pua ya kiboko yapo kwa upande wa juu ya kichwa na hii inamsaidia kuona na kupumua hasa pale anapokuwa kiwiliwili kimezama ndani ya maji na kutoa kichwa juu ya maji.

Macho yake yana utandu wenye kuonesha, ambao humuwezesha kufumbua macho na kuona hata awapo ndani ya maji.

Viboko wanaishi kwa makundi kati ya 10 hadi 30 au zaidi kidogo ambapo kundi hilo huongozwa na dume mtawala kwa kipindi hicho na ndio mwenye uhuru wakupanda majike wote wapatikanao kwenye kundi.

Viboko hutumia muda wa usiku kutafuta chakula na si mchana na wanaweza kutembea hadi kilometa 10 wakiwa wanakula tu.

Licha ya kuwa na maumbile makubwa ya mwili, kiboko ana uwezo wa kukimbia kwa umbali wa kilometa 23km kwa saa.

Kiboko jike huzaa kila baada ya miaka miwili na umri wa kiboko una kadiriwa kuwa miaka 35 – 40 wakati mwingine anaweza fikisha hata miaka 50.

Viboko hawa wameonekana mto Ruaha mkuu kwenye hifadhi ya MBOMIPA
(Matumizi Bora Ya MaliasiIi Idodi na Pawaga) iliyopo katika Mkoa wa Iringa.

Likes:
0 0
Views:
750
Article Tags:
Article Categories:
Uncategorized